1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaChina

China yasema Marekani yaeneza uvumi kuhusu kituo cha ujasusi

Tatu Karema
9 Juni 2023

Serikali ya Cuba imekanusha ripoti ya habari za Marekani kwamba imefikia makubaliano na China kujenga kituo cha ujasusi wa teknolojia nchini Cuba

China I Wang Wenbin I Sprecher des chinesischen Außenministeriums
Picha: Kyodo/picture alliance

Likitaja maafisa wa Marekani wanaofahamu intelijensia ilioainishwa, jarida la Wall Street limesema kuwekwa kwa teknolojia ya ujasusi kama hiyo kungeiwezesha China kukusanya mawasiliano ya kielektroniki kutoka Kusini Mashariki mwa Marekani, ambayo ni makao ya vituo vingi vya jeshi la Marekani pamoja na kufuatilia safari za Meli. Ripoti hizo zinasema kuwa China na Cuba zimeingia katika mkataba wa siri wa kituo hicho cha ujasusi kinachotarajiwa kujengwa katika kisiwa cha Caribbean ambacho kinaweza kufuatilia mawasiliano katika eneo hilo la Kusini Mashariki mwa Marekani.

China yadaiwa kuilipa Cuba mabilioni ya dola

Eneo hilo linajumuisha makao makuu ya kamandi za kijeshi za Kusini na Kati mwa Marekani ambazo zote ziko katika jimbo la Florida. Jarida hilo limeendelea kusema kuwa China itailipa Cuba mabilioni ya dola kuwezesha kujengwa kwa kituo hicho huku likinukuu maafisa wakuu wa Marekani ambao hawakutajwa majina.

Lakini katika taarifa kwa vyombo vya habari, naibu waziri wa mambo ya nje wa Cuba Fernandez de Cossio, alizitaja ripoti hizo kuwa zisizokuwa na msingi. Amesema Cuba inakataa uwepo wa vikosi vyote vyote vya wanajeshi wa kigeni ikiwa ni pamoja na vituo vingi vya kijeshi vya Marekani na wanajeshi wake.

Wang Wenbin asema hafahamu kuhusu suala hilo la kituo cha ujasusi

​​​​​​John Kirby - Msemaji wa usalama wa kitaifa wa White HousePicha: Carolina Chimoy/DW

Wakati huo huo, katika mkutano na wanahabari, alipoulizwa kuhusu kituo hicho kinachodaiwa kuwa ni cha kijasusi, msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya China Wang Wenbin alisema hafahamu kuhusu suala hilo la kituo cha ujasusi kabla ya kukosoa sera ya Marekani kuhusu Cuba. Wang ameongeza kuwa kama inavyojulikana, uenezaji uvumi na kashfa ni mbinu ya kawaida ya Marekani, na muingilio wa masuala ya ndani ya mataifa mengine ni haiba yake. Kiongozi huyo ameongeza kwamba Marekani inapaswa kujitafakari na kukoma kuingilia masuala ya ndani ya Cuba chini ya kisingizio cha uhuru na demokrasia na kufutilia mbali mara moja vikwazo vya kiuchumi, kibiashara na kifedha dhidi ya Cuba.

Msemaji wa usalama wa kitaifa wa White House John Kirby asema ripoti hio sio sahihi.

Huku hayo yakijiri, msemaji wa usalama wa kitaifa wa White House John Kirby, ameliambia shirika la MSNBC kwamba ameona ripoti ya jarida hilo na kwamba sio sahihi. Kirby ameongeza kuwa kile anachoweza kusema ni kwamba wamekuwa na wasiwasi tangu siku ya kwanza ya uongozi ulioko madarakani kuhusu ushawishi wa China na shughuli zake kote duniani hasa katika eneo hilo, akisema kuwa kwa karibu suala hilo.